Monday, August 12, 2013

HII KALI::: Bilionea Msuya kuzikwa leo, jeneza lafunguliwa kwa ‘rimoti’


Arusha. Mazishi ya kifahari yanaandaliwa na familia ya marehemu Erasto Msuya, huku ikielezwa kuwa jeneza litakalotumika kubeba mwili wake linafunguka kwa kutumia ‘rimoti’.
Msuya aliyeuawa wiki iliyopita, anazikwa leo huku familia ikitangaza kutokulipiza kisasi kwa waliohusika, badala yake wamemwachia Mungu.
Kinachovutia katika msiba huo ni jeneza lililobeba mwili wa mfanyabiashara huyo lililoagizwa Nairobi, la aina yake huku likifunguliwa kwa kutumia ‘rimoti’.
Jeneza hilo lililoagizwa kutoka Kampuni ya Montezuma & Monalisa Funeral Home, linafunguliwa kwa kubonyeza kifaa maalumu hata mhusika anapokuwa mbali.
Hali hiyo ilionekana kuwaacha na mshangao maelfu ya waombolezaji waliofika kuaga mwili wakati wa ibada iliyofanyika nyumbani kwake, Kwa Iddi, wilayani Arumeru.
Mfanyabiashara huyo aliyeuawa kwa kumiminiwa risasi zaidi ya 20 na watu wasiojulikana, anazikwa leo nyumbani kwao eneo la Kairo Mirerani, Wilaya ya Simanjiro, mkoani Manyara.
Kaka wa marehemu, Israel Msuya, alisema jana kuwa mazishi hayo yatafanyika makaburi ya familia ya mzee Elisaria Msuya ‘Kikaango’, baba wa marehemu Erasto.
Kwa mujibu wa Kamati ya Maandalizi ya mazishi hayo inayoongozwa na kaka mkubwa wa familia ya Msuya, Gady, zaidi ya Sh100 milioni zimepangwa kugharimia shughuli za maombolezo na mazishi.
Jeneza na gari maalumu la kubebea mwili wa marehemu yameagizwa kutoka Kampuni ya Montezuma & Monalisa Funeral Home ya Nairobi, Kenya kwa gharama ya Sh8 milioni.
Chakula, vinywaji, mapambo na magari ya kukodishwa kutoka Arusha kwenda Mirerani na kurudi yanatarajiwa kugharimu zaidi ya Sh80 milioni.
Katika hatua nyingine, polisi mkoani Arusha imeendelea kuwahoji wafanyabiashara maarufu wa madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani, wilayani Simanjiro, wakidaiwa kuhusika na kifo hicho.
Habari zilizopatikana jana zinadai mfanyabiashara mmoja kijana ambaye aliibuka ghafla kuwa tajiri mkubwa kutokana na biashara ya madini ya Tanzanite, anashikiliwa Arusha kwa mahojiano.
Jana, kwenye viunga vya Mji wa Mirerani watu walitangaziwa kuwa mfanyabiashara huyo, alikuwa anashikiliwa kwa mahojiano kuhusiana na kifo hicho.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, hakupatikana mara moja kuelezea suala hilo kwani simu yake ilipopigwa ilikuwa haipatikani.
Marehemu ameacha mke na watoto wanne, huku akiacha rasilimali nyingi ikiwamo jumba la kifahari lililopo Sakina kwa Idd, hoteli maarufu za SG Resort na Mezza Luna zilizopo Arusha.

No comments:

Post a Comment